DAWASA MTAA KWA MTAA YAMALIZIKA KWA KISHINDO KINONDONI

Zaidi ya Wateja 3000 waboreshewa huduma za Maji Goba na Wazo
Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) imehitimisha kwa kishindo kampeni ya DAWASA mtaa kwa mtaa katika kata za Goba na Wazo wilaya ya Kinondoni ambapo wateja zaidi ya 3000 wamefikiwa na kuhudumiwa.
Akizungumza wakati wa kuhitimisha kampeni hiyo kwa naiba ya Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu Ndugu Paul Sulley ameeleza kuwa kupitia kampeni hiyo wateja 3000 wa kata za Goba na Wazo wamefikiwa na kutatuliwa changamoto za kihuduma ambazo ni pamoja na kurejeshewa huduma kwa wateja waliositishiwa kutokana na madeni kwa kuwapa mikataba ya kulipa kidogo kidogo na kufanikiwa kuunganishwa huduma ya maji kwa wateja wapya waliokamilisha taratibu za kupata huduma.
"Zoezi hii limerudisha tabasamu kwa wakazi wa Goba na Wazo, zoezi lilifanyika siku tatu kuanzia Septemba 19-21 na lilianza kwa kuweka Dawati la huduma na leo limehitimishwa kwa Watumishi wa ofisi kuu za Mamlaka wa Mwananyamala na Ubungo kupita nyumba kwa nyumba kuhudumia Wananchi." alisema Sulley.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa huduma kwa wateja CPA (T) Ritamary Lwabulinda ameeleza kuwa zoezi hilo ni endelevu na limesaidia kuwafikia wateja na kuwasikiliza kwa dhumuni la kuboresha huduma.
"Tumepata ushirikiano mkubwa kwa wateja wetu wametueleza changamoto mbalimbali ikiwemo ikiwemo wizi wa mita unaoendelea katika maeneo yao na sisi tumewapa elimu ya jinsi ya kuzilinda kwa kuzijengea kisasa ili zisiweze kuibiwa" aliongezea Rithamary Lwabulinda
Gwanta Mwalopo mkazi wa mtaa wa Mivumoni amesema ujio wa DAWASA ni neema kwao ambapo wameweza kutatuliwa changamoto zao.
"Ujio wa DAWASA leo na vifaa vyao tumeona wameziba mivujo iliyokuwa inaharibu barabara zetu lakini pia wametupa mawasiliano yao ikitokea changamoto nyingine tuweze kuwasiliana nao" alisema Bi. Mwalopo
Zoezi la DAWASA mtaa kwa mtaa ni endelevu lenye lengo la kuwafikia wananchi katika maeneo yao ili kuwasikiliza na kujenga mahusiano bora katika wananchi na Mamlaka.