BWAWA LA KIDUNDA KUKAMILIKA DESEMBA 2026, KUONDOA NAKISI YA UPUNGUFU WA MAJI
Msemaji Mkuu wa Serikali, ambae pia ni Katibu Mkuu, Wizara ya Habari Sanaa Utamaduni na Michezo ndugu Gerson Msigwa katika Taarifa yake ya Msemaji Mkuu wa Serikali ameeleza kuwa kukamilika kwa ujenzi wa Bwawa la Kidunda Mkoani Morogoro ambao umefikia asilimia 50 ya utekelezaji kutaenda kuondoa nakisi ya upungufu wa maji kwa wakazi wa Jiji na Dar Es Salaam na Mkoa wa Pwani hususani kipindi cha ukame.
"Mradi huu umesanifiwa toka mwaka 1961, baada ya sintofahamu nyingi katika kuutekeleza, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Daktari Samia Suluhu Hassan alipoingia madarakani alisema sasa maneno yanatosha tukaanze utekelezaji wa mradi huu, na ndio alipoidhinisha fedha kiasi cha shilingi bilioni 336 zitumike" ameeleza ndugu Msigwa.
Msigwa ameongeza kuwa Jiji la Dar Es Salaam lenye wakazi zaidi ya Milioni 7 ni muhimu sana kiuchumi katika nchi yetu hivyo linapaswa kuwa na chanzo cha uhakika cha maji ili kuchochea shughuli za kiuchumi.
"Katika Bwawa hili tutahifadhi maji Lita bilioni 190, tutatumia maji lita bilioni 2 tu kwa siku, hatua hii itawezesha mitambo ya kuchakata maji ya DAWASA kuwa na uhakika wa maji kwa kipindi chote cha mwaka, ni lazima watu hawa wa Jiji la Dar Es Salaam na Pwani tuwapatie uhakika wa Majisafi na Salama" Ameeleza Msigwa.
Katika Taarifa hiyo ya Msemaji Mkuu wa Serikali, Msigwa ameeleza kuwa Serikali kupitia dira ya Taifa ya mwaka 2025-2050 itayoanza kutekelezwa ifikapo tarehe 1, Julai 2026 imedhamiria kila mwananchi kupata Majisafi na Salama kwa asilimia 100.
