GOLANI MAJI NI MWA MWA MWAAA
Wakazi wa Mtaa wa Golani, Kata ya Kimara, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam wameishukuru Serikali kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) baada ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa kituo cha kusukuma maji (Booster Pump), ambao umeondoa changamoto ya upatikanaji wa maji iliyodumu kwa muda mrefu katika eneo hilo.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Mavurunza, Ally Salehe, amesema mradi huo umeleta nafuu kubwa kwa wakazi ambao kwa miaka mingi walikabiliwa na uhaba wa maji safi na salama.
Amesema kukamilika kwa mradi huo ni matokeo ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha Wananchi wanapata huduma muhimu za maji karibu na maeneo yao.
"Tunamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutenga fedha za kukamilisha mradi huu, usimamizi mzuri wa DAWASA ambao sasa matokeo yake yanaonekana wazi. Leo hii huduma ya maji inapatikana katika maeneo mengi ya Golani na hii ndiyo ilikuwa ndoto ya wananchi wetu kwa muda mrefu," amesema Salehe.
Aidha, amewahimiza wananchi kushiriki kulinda miundombinu ya maji ili huduma hiyo iwe endelevu na kuwahudumia wakazi kwa muda mrefu.
Mary Zidadu, mkazi wa Golani Millenium amesema kabla ya utekelezaji wa mradi huo wakazi walilazimika kutembea umbali mrefu kufuata maji kutoka kwenye visima ambavyo havikuwa salama kwa matumizi ya binadamu.
Amesema hali hiyo sasa imebadilika baada ya wananchi kuanza kupata maji safi na salama kutoka DAWASA.
"Kwa muda mrefu tulikuwa tunatembea hadi kilomita sita kufuata maji ya visimani ambayo hayakuwa salama. Leo tunapata maji safi na salama karibu na makazi yetu. Tunawashukuru sana DAWASA kwa kutatua changamoto hii ya muda mrefu," amesema Zidadu.
Mradi wa kituo cha kusukuma maji cha Golani umetekelezwa na DAWASA kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 291 na unatarajiwa kuhudumia zaidi ya wakazi 5,000 wa maeneo ya Golani, Saranga, Ukombozi, Mavurunza, Mnazi Mmoja na Mnara wa Voda.
